Kwa kifupi Shirika limeitikia wito wa Serikali wa kuhakikisha mashirika yanayopokea ruzuku toka Serikalini yanajijengea uwezo wa kujitegemea kwa kupunguza utegemezi serikalini. Pia mashirika ya aina hiyo yanawajibika kuendesha tafiti na kuendeleza teknolojia za gharama nafuu zinazolengwa kuwasaidia watanzania kujijengea uwezo wa kujikwamua kiuchumi.
Katika kipindi cha miaka 10 ya Serikali ya awamu ya nne Shirika la Mzinga limefanya yafuatayo:-

1.  Uzalishaji wa Baruti
Shirika limezalisha baruti na kuanzisha vituo vya uuzaji wa baruti hizo katika maeneo ya Mererani (Simanjiro), Arusha, Shinyanga na Mpanda kwa lengo la kuwarahisishia wachimbaji wadogo kupata nyenzo hiyo inayowasaidia katika shughuli za uchimbaji madini badala ya kuwaachia wachimbaji wakubwa uwezo huo peke yao. Usafirishaji wa baruti ni hatari kubwa kwa maisha, na sheria inazuia wachimbaji wadogo kufanya hivyo kwa ajili ya usalama wa maisha yao. Shirika linawafikishia nyenzo hiyo huko waliko, na juhudi za kufikisha nyenzo hiyo kwenye maeneo mengine zinakofanyika shughuli za uchimbaji zinafanyika.

2.  Utengenezaji Samani
Shirika limeitikia wito wa Serikali wa kuzalisha samani imara zinazotokana na mbao ngumu nchini kwa ajili ya matumizi serikalini kwa lengo la kupunguza na hatimaye kuondoa matumizi ya samani dhaifu zinazotengenezwa nchi za nje. Samani hizo za nje zinaligharimu taifa fedha nyingi lakini hazidumu ikilinganishwa na samani zinazozalishwa hivi sasa na Shirika la Mzinga kwa kutumia mbao halisi. Shirika limewekeza katika teknolojia ya kisasa katika kutekeleza jukumu hili.

3.  Mashine za kuchakata mazao
Shirika limejikita pia katika kuzalisha mashine mbalimbali za kuchakata mazao zikiwemo mashine za kukoboa na kusaga chakula cha binadamu, mashine za kusaga na kuchanganya chakula cha mifugo, mashine za kukamua alizeti, na nyingine nyingi. Kote zilikouzwa, mashine hizo zimetengeza ajira za moja kwa moja na zisizo za moja kwa moja kwa watu na vikundi vinavyoshiriki kuzifanya mashine hizo kuzalisha. Changamoto kubwa katika eneo hili ni uwezo mdogo wa wananchi kununua mashine hizo. Shirika linawashauri wananchi kujiunga katika vikundi na kuwasiliana na Shirika juu ya namna bora ya kujipatia mikopo kutoka katika mabenki itakayowawezesha kununua teknolojia hizo.

4.  Shughuli za ujenzi
Mwaka 2012 Shirika lilianzisha kampuni tanzu ya ujenzi (Mzinga Holdings) ambayo katika kipindi cha miaka mitatu imeweza kupewa na kukamilisha miradi mingi kwa lengo la kulipunguzia Shirika mama utegemezi kwenye ruzuku toka serikalini. Baadhi ya miradi hiyo ni pamoja na ujenzi wa soko la Kemondo, (mkoani Kagera), Ujenzi wa hostel ya Masista wa St. Theresa (Kashozi, Kagera), Ujenzi wa kiwanda cha maji cha Bunena (Bukoba), Ujenzi wa daraja la Mabwepande (Dar es Salaam), Ujenzi na ukarabati wa majengo ‘Air Force Station’ (AFS, Mwanza), ukarabati wa nyumba 40 za Jeshi huko Kitangiri (Mwanza), ujenzi wa nyumba za halmashauri za Masasi na Morogoro, ujenzi wa hospitali ya wilaya (Mkundi, Morogoro) na ujenzi wa mazingira na uwekaji samani kwenye makao ya kudumu ya Chuo cha Ukamanda na Unadhimu (Tengeru, Arusha).

5.  Utafiti
Shirika linashirikiana na taasisi mbalimbali za utafiti katika kuendesha tafiti na kutengeneza vifaa vinavyotokana na tafiti hizo. Baadhi ya taasisi hizo ni pamoja na Chuo kikuu cha Dar es Salaam, na Tume ya Taifa ya Sayansi na Teknolojia (COSTECH), CoET, CAMARTEC,
TIRDO n.k.

Kwa maelezo ya kina ona powerpoint presentation ifuatayo:

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...