Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo akiongozana na baadhi ya viongozi wa makampuni ya mafuta wakati wa ziara ya kukagua matanki ya kuhifadhia mafuta leo jijini Dar es salaam.
 Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo akiongea na baadhi ya viongozi wa makampuni ya mafuta  wakati wa ziara ya kukagua matanki ya kuhifadhia mafuta leo jijini Dar es salaam ili kujionea hali ya upatikanaji wa mafuta ya ndege baada ya kugundulika baadhi ya shehena ya mafuta hayo yaliyoingizwa nchini yalikuwa yamechanganyika na mafuta ya petroli. Kwa picha zaidi BOFYA HAPA
Na Eleuteri Mangi-MAELEZO
Serikali imewatoa hofu na kuwahakikishia Watanzania na abiria wanaotumia usafiri wa anga nchini kwamba mafuta ya ndege yapo ya kutosheleza matumizi kwa muda wa siku 14 wakati shehena nyingine za mafuta hayo zinaendelea kuingia nchini.
Hayo yamesememwa na Waziri wa Nishati na Madini Prof. Sospeter Muhongo alipofanya ziara leo jijini Dar es salaam kukagua matanki ya kuhifadhia mafuta ili kujionea hali ya upatikanaji wa mafuta ya ndege nchini baada ya kugundua baadhi ya shehena ya mafuta hayo yaliyoingizwa nchini yalikuwa yamechanganyika na mafuta ya petroli.
“Mafuta ya ndege yapo na ndege zitaendelea kufanya safari kama ratiba zao zilivyopangwa na Watanzania msiwe na wasiwasi, tumejiridhisha, mafuta yanatosheleza kwa muda wa siku 14 wakati hatua ya shehena nyingine kuingia nchini zinaendelea” alisema Prof. Muhongo.
Ziara hiyo ya Waziri Prof. Muhongo inafuatia kugundulika kwa mafuta ya ndege yaliyoingizwa nchini mapema mwezi Mei mwaka huu, ambayo hayafai kwa matumizi yaliyokusudiwa kutokana na kuchanganywa na mafuta ya petroli.
Aidha, Prof. Muhongo ameitaka kampuni ya Sahara Energy Resources yenye makao yake makuu nchini Nigeria ambayo ndio ilioingiza mafuta hayo nchini, kusimamisha shughuli zake mara moja hadi suala hilo litakapopatiwa ufumbuzi.
Imeonekana si mara ya kwanza kwa kampuni hiyo kuingiza mafuta machafu nchini, hatua iliyomfanya Waziri huyo kuchukua msimamo huo wa Serikali hadi suala hilo litakapopatiwa ufumbuzi.
Akizungumzia hatua hiyo na hali ya mafuta nchini, Kaimu Mkurugenzi Mtendaji Wakala wa Uingizaji Mafuta kwa Pamoja nchini, Michael Mjinja amesema kuwa mafuta ya ndege yapo na yanatosheleza kwa wiki mbili kuanzia sasa.
Mjinja aliongeza kuwa wanakuhakikisha uhaba wa mafuta hayo hautokei tena nchini ambapo wanaendelea kushirikiana na kampuni ya Total na SP Rwanda ambazo hadi sasa ndio zenye mafuta safi yanayokubalika kwa matumizi.
Kwa upande wake Mkurugenzi Mtendaji wa Kampuni ya TIPER iliyoko eneo la Kigamboni jijini Dar es salaam, Stephane Gay amesema kuwa kampuni yake ina nafasi ya kutosha ya kuyahifadhi mafuta yote ambayo hayastahili kutumika ili matanki na mitambo ya kampuni zote zilizopata mafuta hayo yafanyiwe usafi upya tayari kwa kuweka mafuta safi yanayoingia nchini.

Ziara ya Waziri Prof. Muhongo imehusisha kutembelea matanki ya kampuni tano za mafuta ikiwemo Puma, GAPCO, Oil Com, TIPER pamoja na Kampuni ya Oryx Energies. 

Michuzi Blog

Tanzanian blog operating since 2005, covering International news and Local News, including Politics, Fashion, Social Scenes, Interviews, Movies, Events, personalities and anything positive happening worldwide. Written in Swahili and English targeting both Swahili and English readers.

Toa Maoni Yako:

0 comments so far,add yours

Hii ni Blog ya Watanzania popote walipo duniani kwa ajili ya kuhabarisha, kutoa/kupokea taarifa na kuelimisha mambo yote yaliyo chanya kwa Taifa letu. Tafadhali sana unapotoa maoni usichafue hali ya hewa wala usijeruhi hisia za mtu/watu. Kuwa mstaarabu...